Sauli na Wanawe Waanguka Vitani
10 1Wafilisti walipigana na Israeli; watu wa Israeli wakawakimbia, wakaanguka wakiuawa katika mlima Gilboa. 2Wafilisti wakamfuatia Sauli na wanawe kwa bidii, wakawaua Yonathani, Abinadabu, na Malkishua, wana wa Sauli. 3Vita vikawa vikali dhidi ya Sauli; wapiga mishale wakamfikia, nao wakamjeruhi vibaya. 4Sauli akamwambia mchukua silaha wake, "Futa upanga wako, unichome nao, wasije watu hawa wasiotahiriwa wakanidhihaki." Lakini yeye akakataa, kwa maana aliogopa sana. Basi Sauli akautwaa upanga mwenyewe, akauangukia.
5Mchukua silaha wake alipoona ya kuwa Sauli amekufa, naye pia akauangukia upanga wake, akafa. 6Basi Sauli akafa, na wanawe watatu, na watu wote wa nyumba yake wakafa pamoja.
7Watu wa Israeli waliokuwa bondeni walipoona ya kuwa jeshi limekimbia, na Sauli na wanawe wamekufa, wakaziacha miji yao wakakimbia. Nao Wafilisti wakaja, wakakaa humo.
8Siku ya pili yake, Wafilisti walipokuja kuwavua waliokufa nguo, wakamkuta Sauli na wanawe wameanguka katika mlima Gilboa. 9Wakamvua nguo, wakakichukua kichwa chake na silaha zake, wakatuma wajumbe katika nchi yote ya Wafilisti kuitangaza habari hiyo kwa sanamu zao na kwa watu. 10Wakaziweka silaha zake katika hekalu la miungu yao, na kichwa chake wakakikaza katika hekalu la Dagoni.
11Lakini watu wote wa Yabesh-gileadi waliposikia yote ambayo Wafilisti walikuwa wamemtenda Sauli, 12watu wao wote mashujaa wakainuka, wakauchukua mwili wa Sauli na miili ya wanawe, wakaileta Yabeshi, wakaizika mifupa yao chini ya mwaloni ulioko Yabeshi, wakafunga saumu siku saba.
13Basi Sauli akafa kwa sababu ya kukosa uaminifu kwake dhidi ya Baba yetu—hakulishika neno la Baba yetu, hata akauliza shauri kwa mtu apandishaye pepo apate mwongozo. 14Hakumtafuta Baba yetu, kwa hiyo Baba yetu akamwua, akaugeuza ufalme kumpa Daudi mwana wa Yese.