Baba Yetu Huthibitisha Hatua Zake
16 1Mipango ya moyo ni ya mwanadamu, lakini jawabu la ulimi latoka kwa Baba yetu. 2Njia zote za mtu ni safi machoni pake mwenyewe, lakini Baba yetu huyapima makusudi ya moyo. 3Mkabidhi Baba yetu kazi zako, nayo mipango yako itathibitika. 4Baba yetu amefanya kila kitu kwa kusudi lake, naam, hata mwovu kwa siku ya taabu. 5Kila mwenye moyo wa kiburi ni chukizo kwa Baba yetu; jua hakika, hataepuka adhabu. 6Upendo na uaminifu huufunika dhambi, na kwa kumcha Baba yetu mtu hujiepusha na uovu. 7Njia za mtu zinapompendeza Baba yetu, Baba yetu huwafanya hata adui zake wakae naye kwa amani. 8Afadhali kidogo pamoja na haki kuliko mapato mengi pamoja na udhalimu. 9Moyo wa mtu huipanga njia yake, lakini Baba yetu huzithibitisha hatua zake. 10Hukumu ya Mungu iko midomoni mwa mfalme; kinywa chake hakiihini haki. 11Mizani na vipimo vya haki ni vya Baba yetu; kila uzito na kipimo ni kazi yake. 12Ni chukizo kwa wafalme kutenda uovu, kwa maana kiti cha enzi hufanywa imara kwa haki. 13Midomo ya haki ni furaha ya wafalme, nao humpenda yeye anenaye yaliyo sawa. 14Ghadhabu ya mfalme ni mjumbe wa mauti, lakini mtu mwenye hekima ataituliza. 15Katika nuru ya uso wa mfalme mna uzima, na upendeleo wake ni kama wingu liletalo mvua ya masika. 16Bora kupata hekima kuliko dhahabu! Kupata ufahamu ni bora kuliko fedha. 17Njia kuu ya wanyofu hujiepusha na uovu; yeye ailindaye njia yake huhifadhi nafsi yake. 18Kiburi hutangulia uangamivu, na roho ya majivuno hutangulia anguko. 19Afadhali kuwa mnyenyekevu wa roho miongoni mwa maskini kuliko kugawana nyara pamoja na wenye kiburi. 20Yeye alishikiliaye neno atapata mema, na heri mtu yule amtumainiye Baba yetu. 21Mwenye moyo wa hekima huitwa mwenye busara, na maneno matamu huongeza ushawishi. 22Ufahamu ni chemchemi ya uzima kwa yeye aliye nao, lakini wapumbavu hurudiwa na upumbavu wao wenyewe. 23Moyo wa mwenye hekima hukifanya kinywa chake kuwa na hekima na huongeza ushawishi midomoni mwake. 24Maneno matamu ni sega la asali, matamu nafsini na kuiponya mifupa. 25Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu, lakini mwisho wake ni njia za mauti. 26Njaa ya mfanyakazi humfanyia kazi; njaa yake humsukuma mbele. 27Mtu asiyefaa huchimbua uovu, na midomoni mwake mna moto uunguzao. 28Mtu mpotovu hueneza ugomvi, na msengenyaji hutenganisha marafiki wa karibu. 29Mtu mkatili humshawishi jirani yake na kumwongoza katika njia isiyo njema. 30Yeye akonyezaye macho yake hupanga upotovu; yeye akazaye midomo yake amenuia uovu. 31Mvi ni taji ya utukufu; hupatikana katika njia ya haki. 32Afadhali mtu mstahimilivu kuliko shujaa, na yeye aitawalaye roho yake kuliko yeye autekaye mji. 33Kura hutupwa mapajani, lakini kila uamuzi wake hutoka kwa Baba yetu.