Wema wa Daudi Ulipwa kwa Aibu
19 1Baada ya muda, Nahashi mfalme wa Waamoni akafa, na mwanawe akawa mfalme mahali pake. 2Daudi akasema, "Nitamtendea wema Hanuni mwana wa Nahashi, kwa kuwa baba yake alinitendea wema." Basi Daudi akatuma wajumbe kumfariji kwa ajili ya baba yake. Lakini watumishi wa Daudi walipofika katika nchi ya Waamoni, kwa Hanuni, ili kumfariji, 3wakuu wa Amoni wakamwambia Hanuni, "Je, wewe wadhani kweli Daudi anamheshimu baba yako kwa kukutumia wafariji? Je, watumishi wake hawakuja kwako ili kuipeleleza nchi, kuipindua, na kuichunguza?" 4Hanuni akawakamata watumishi wa Daudi, akawanyoa, akayakata mavazi yao katikati hadi kwenye viuno, akawaacha waende zao. 5Walipomwambia Daudi habari za watu hao, akatuma wajumbe kuwalaki, kwa kuwa walikuwa wameaibika sana. Mfalme akasema, "Kaeni Yeriko mpaka ndevu zenu ziote, kisha mrudi."
6Waamoni walipoona ya kuwa wamekuwa chukizo kwa Daudi, Hanuni na Waamoni wakapeleka takriban tani thelathini na nane za fedha ili kukodi magari ya vita na wapanda farasi kutoka Aram-naharaimu, Aram-maaka, na Soba. 7Wakakodi magari ya vita 32,000, pamoja na mfalme wa Maaka na majeshi yake, waliokuja na kupiga kambi mkabala na Medeba. Waamoni wakakusanyika kutoka miji yao, wakatoka kwenda vitani. 8Daudi aliposikia habari hizo, akamtuma Yoabu pamoja na jeshi lote la watu mashujaa. 9Waamoni wakatoka nje, wakapanga safu za vita penye lango la mji, huku wale wafalme waliokuja wakiwa peke yao uwandani.
10Yoabu alipoona ya kuwa vita vimepangwa dhidi yake mbele na nyuma, akachagua askari walio bora wa Israeli, akawapanga wakabiliane na Waaramu. 11Wale askari waliobaki akawaweka chini ya Abishai ndugu yake, nao wakajipanga dhidi ya Waamoni. 12Yoabu akasema, "Ikiwa Waaramu watanishinda nguvu, uniokoe; na ikiwa Waamoni watakushinda nguvu wewe, nitakuokoa. 13Uwe hodari; tupigane kwa ushujaa kwa ajili ya watu wetu na kwa ajili ya miji ya Baba yetu, naye Baba yetu na afanye lililo jema machoni pake."
14Ndipo Yoabu na askari waliokuwa pamoja naye wakasogea mbele ili kupigana na Waaramu, nao wakakimbia mbele yake. 15Waamoni walipoona ya kuwa Waaramu wamekimbia, nao pia wakakimbia mbele ya Abishai ndugu yake, wakaingia mjini. Ndipo Yoabu akaja Yerusalemu.
16Waaramu walipoona ya kuwa Israeli imewashinda, wakatuma wajumbe, wakawaleta Waaramu waliokuwa ng'ambo ya Mto Frati, wakiwa na Shofaki, jemadari wa jeshi la Hadadezeri, mbele yao. 17Daudi akaambiwa; akakusanya Israeli wote, akavuka Yordani, akawaendea, akapanga safu za vita. Daudi akapanga safu za vita dhidi ya Waaramu, nao wakapigana naye. 18Waaramu wakakimbia mbele ya Israeli. Daudi akawaua wapanda magari ya vita 7,000 na askari wa miguu 40,000, kisha akamwua Shofaki, jemadari wa jeshi lao. 19Watumishi wa Hadadezeri walipoona ya kuwa Israeli imewashinda, wakafanya amani na Daudi, wakamtumikia. Waaramu hawakuwa tayari tena kuwasaidia Waamoni.