Elifazi Anena Tena
22 1Ndipo Elifazi Mtemani akajibu: 2"Je, mwanadamu aweza kumfaidia Mungu? Hakika mtu mwenye hekima hujifaidia mwenyewe tu. 3Je, ni furaha yoyote kwa Mwenyezi ikiwa wewe ni mwenye haki, au ni faida yoyote kwake ikiwa unaishi bila lawama? 4Je, ni kwa sababu ya uchaji wako ndipo anakukemea na kukuleta hukumuni? 5Je, uovu wako si mkuu? Je, dhambi zako si zisizo na mwisho? 6Kwa maana uliwadai ndugu zako rehani bila sababu na kuwavua nguo walio uchi. 7Hukumpa maji aliyechoka anywe, nawe ulimzuia mkate mwenye njaa. 8Mtu mwenye nguvu aliimiliki nchi, na aliyependelewa aliishi ndani yake. a a v8 Elifazi anadokeza kuwa Ayubu aliichukulia nchi kuwa mali ya wenye nguvu peke yao, akiwaacha maskini bila kitu. 9Uliwaondoa wajane mikono mitupu na kuivunja mikono ya yatima. 10Ndiyo maana mitego imekuzunguka, na hofu ya ghafla inakulemea; 11au giza, hata usiweze kuona, na mafuriko ya maji yanakufunika. 12Je, Mungu hayuko katika vilele vya mbingu? Tazama jinsi nyota zilizo juu zaidi zilivyo juu! 13Lakini wewe wasema, 'Mungu anajua nini? Je, aweza kuhukumu katika giza nene namna hii? 14Mawingu mazito yanamfunika hata asiweze kuona, naye anatembea juu ya anga la mbingu.' 15Je, utaishika njia ya kale ambayo watu waovu waliitembea? 16Walinyakuliwa kabla ya wakati wao, msingi wao ukasombwa na mafuriko. 17Walimwambia Mungu, 'Tuache! Mwenyezi aweza kutufanya nini?' 18Lakini ni yeye aliyezijaza nyumba zao mema—hivyo mimi sitaki kuwa na sehemu yoyote katika mipango ya waovu. 19Wenye haki wanaliona na kufurahi; wasio na hatia wanawadhihaki waovu, wakisema, 20'Hakika adui zetu wameangamizwa, na moto umeteketeza walichokiacha.' 21Nyenyekea kwa Mungu sasa na uwe na amani naye; kwa njia hii mema yatakujia. 22Pokea mafundisho kutoka kinywani mwake, na uyahifadhi maneno yake moyoni mwako. 23Ukimrudia Mwenyezi utarejeshwa; ukiuondoa udhalimu mbali na nyumba yako, 24na kuiweka dhahabu yako mavumbini, dhahabu ya Ofiri kati ya mawe ya bondeni, b b v24 Ofiri ilikuwa maarufu katika ulimwengu wa kale kama chanzo cha dhahabu iliyo bora kabisa. 25ndipo Mwenyezi mwenyewe atakuwa dhahabu yako, fedha yako ya thamani. 26Ndipo utakapofurahia katika Mwenyezi na kumwinulia Mungu uso wako. 27Utamwomba, naye atakusikia, nawe utazitimiza nadhiri zako. 28Utakachoamua kitatimizwa, na nuru itaangaza juu ya njia zako. 29Wengine watakaposhushwa nawe useme, 'Wainueni!', yeye atawaokoa walioinama. 30Atamwokoa hata yule asiye na hatia, ambaye ataokolewa kwa usafi wa mikono yako."