Maneno ya Uzembe, Ulimi Uponyao
12 1Apendaye adabu hupenda maarifa, bali achukiaye kurekebishwa ni mpumbavu. 2Mtu mwema hupata kibali kwa Baba yetu, bali yeye humhukumu mtu afanyaye hila za uovu. 3Hakuna mtu awezaye kuimarishwa kwa uovu, bali mzizi wa wenye haki hautaondolewa kamwe. 4Mke mwenye tabia adhimu ni taji ya mumewe, bali aletaye aibu ni kama uozo mifupani mwake. 5Mipango ya wenye haki ni ya adili, bali mashauri ya waovu ni ya udanganyifu. 6Maneno ya waovu huotea ili kumwaga damu, bali usemi wa wanyofu huwaokoa wasio na hatia. 7Waovu hupinduliwa wasiwepo tena, bali nyumba ya wenye haki itasimama. 8Mtu husifiwa kwa kadiri ya busara yake, bali mwenye moyo uliopotoka hudharauliwa. 9Afadhali kuwa mnyonge na kuwa na mtumishi kuliko kujidai ukuu na kukosa chakula. 10Mwenye haki hujali mahitaji ya wanyama wake, bali hata huruma ya waovu ni ukatili. 11Alimaye shamba lake atakuwa na chakula tele, bali afuataye mambo ya ubatili hana akili. 12Waovu hutamani nyara za watu wabaya, bali mzizi wa wenye haki huzaa matunda. 13Mtu mbaya hunaswa kwa maneno yake ya dhambi, bali mwenye haki huokoka kutoka taabuni. 14Kwa tunda la maneno yake mtu hushibishwa mema, na kazi ya mikono yake humrudia kama thawabu. 15Njia ya mpumbavu huonekana sawa machoni pake mwenyewe, bali mwenye hekima husikiliza shauri. 16Mpumbavu huonyesha hasira yake papo hapo, bali mwenye busara hupuuza tukano. 17Anenaye kweli hutoa ushuhuda wa haki, bali shahidi wa uongo husema uongo. 18Maneno ya uzembe huchoma kama upanga, bali ulimi wa mwenye hekima huleta uponyaji. 19Midomo ya kweli hudumu milele, bali ulimi wa uongo hukaa kitambo kidogo tu. 20Hila hujaza mioyo ya wale wapangao uovu, bali furaha ni ya wale waenezao amani. 21Hakuna baa limpatalo mwenye haki, bali waovu wamejaa taabu. 22Midomo ya uongo ni chukizo kwa Baba yetu, bali watendao kwa uaminifu ni furaha yake. 23Mwenye busara huficha maarifa yake, bali moyo wa wapumbavu hupayuka upumbavu. 24Mikono yenye bidii itatawala, bali uvivu huishia katika kazi ya kulazimishwa. 25Wasiwasi hulemea moyo, bali neno la wema hufurahisha. 26Mwenye haki humwongoza jirani yake, bali njia ya waovu huwapotosha. 27Mvivu haoki mawindo yake, bali mwenye bidii huthamini mali zake. 28Katika njia ya haki kuna uzima, na katika njia hiyo hakuna mauti.