Sikilizeni, Watoto Wangu
4 1Sikilizeni, watoto wangu, mafundisho ya baba; sikilizeni kwa makini, mpate ufahamu. 2Ninawapa mafundisho mema, basi msiache maagizo yangu. 3Kwa maana mimi nami nilikuwa mwana kwa baba yangu, mpole na mpendwa wa pekee wa mama yangu. 4Alinifundisha, akaniambia, "Moyo wako uyashike maneno yangu; zishike amri zangu nawe utaishi. 5Jipatie hekima, jipatie ufahamu; usisahau, wala usiyaache maneno ya kinywa changu. 6Usimwache, naye atakulinda; umpende, naye atakutunza. 7Mwanzo wa hekima ni huu: jipatie hekima; na kwa vyote uvipatavyo, jipatie ufahamu. 8Mthamini, naye atakuinua juu; mkumbatie, naye atakuletea heshima. 9Atakuvika kichwani chako taji la neema; atakukabidhi taji la utukufu."
10Sikiliza, mwanangu, uyapokee maneno yangu, nayo miaka ya maisha yako itakuwa mingi. 11Nimekufundisha njia ya hekima; nimekuongoza katika mapito yaliyonyoka. 12Utembeapo, hatua zako hazitazuiliwa; na ukimbiapo, hutajikwaa. 13Yashike mafundisho, usiyaache; yalinde, kwa maana ni uhai wako.
14Usiuguse mguu wako katika njia ya waovu, wala usitembee katika njia ya watendao mabaya. 15Iepuke, usiipite; geuka na kuiacha, upite mbali. 16Kwa maana hawawezi kulala usingizi wasipotenda ubaya; usingizi wao huondolewa wasipomkwaza mtu. 17Wao hula mkate wa uovu na kunywa divai ya udhalimu.
18Bali njia ya wenye haki ni kama mwanga wa mapambazuko, unaozidi kung'aa hata mchana mkamilifu. 19Njia ya waovu ni kama giza nene; hawajui kinachowakwaza.
20Mwanangu, yasikilize maneno yangu; utege sikio lako kwa misemo yangu. 21Yasiondoke machoni pako kamwe; yahifadhi ndani sana ya moyo wako. 22Kwa maana ni uhai kwa wale wayapatao, na afya kwa mwili wao wote.
23Zaidi ya yote, uulinde moyo wako, kwa maana yote uyatendayo hutoka humo. 24Uondoe usemi wa upotovu kinywani mwako, na midomo ya udanganyifu iweke mbali nawe. 25Macho yako na yatazame mbele moja kwa moja; kaza macho yako mbele yako. 26Fikiria kwa makini njia ya miguu yako, nazo njia zako zote zitakuwa imara. 27Usigeuke kuume wala kushoto; ukiepushe mguu wako na uovu.