Esta Awaombea Watu Wake
7 1Basi mfalme na Hamani wakaja kunywa pamoja na Malkia Esta. 2Siku ya pili, walipokuwa wakinywa mvinyo, mfalme akamwuliza tena, "Ni haja gani yako, Malkia Esta? Utapewa. Ombi lako ni nini? Hata nusu ya ufalme—utafanyiwa."
3Malkia Esta akajibu, "Ikiwa nimepata kibali machoni pako, ee mfalme, na ikimpendeza mfalme, nipe uhai wangu kwa haja yangu, na watu wangu kwa ombi langu. 4Kwa maana tumeuzwa, mimi na watu wangu, ili tuangamizwe, tuuawe, na kufutiliwa mbali. Kama tungeuzwa tu kuwa watumwa wanaume na wanawake, ningenyamaza; taabu kama hiyo isingestahili kumsumbua mfalme."
5Ndipo Mfalme Ahasuero akamwambia Malkia Esta, "Ni nani huyo, na yuko wapi, athubutuye kutenda jambo hili?"
6Esta akasema, "Adui na mtesi—ni Hamani huyu mwovu!" Hamani akaogopa sana mbele ya mfalme na malkia.
7Kwa hasira, mfalme akainuka kutoka pale walipokunywa mvinyo, akaenda bustani ya jumba la kifalme, huku Hamani akibaki ili kumsihi Malkia Esta amwokoe uhai wake, kwa kuwa aliona ya kwamba mfalme amekusudia kumwangamiza. 8Mfalme akarudi kutoka bustani ya jumba la kifalme mpaka ukumbi wa karamu. Hamani alikuwa ameanguka juu ya kiti alichokuwa amekaa Esta. Mfalme akasema, "Je, atamdhulumu hata malkia nikiwapo mimi nyumbani?" Maneno hayo yalipotoka kinywani mwa mfalme, wakaufunika uso wa Hamani. a a v8 Kuufunika uso wa mtu aliyehukumiwa kulikuwa ni ishara ya kale kwamba hatima yake imethibitika—alikuwa kama mtu aliyekwisha kufa.
9Harbona, mmoja wa matowashi wa mfalme, akasema, "Tazama, ile miti ya kunyongea yenye urefu wa dhiraa hamsini, ambayo Hamani aliitengeneza kwa ajili ya Mordekai, aliyenena kwa faida ya mfalme, imesimama nyumbani kwa Hamani." Mfalme akasema, "Mtundikeni juu yake."
10Basi wakamtundika Hamani juu ya ile miti aliyokuwa ameiandaa kwa ajili ya Mordekai, na ghadhabu ya mfalme ikatulia.